Wednesday 7 December 2016

Donald Trump ashinda tuzo ya mtu mashuhuri wa Time mwaka 2016

Rais mteule wa Marekani Donald Trump ametangazwa kuwa mtu mashuhuri zaidi duniani wa mwaka 2016 na jarida la Time.
Tajiri huyo alipokezwa taji hilo kutokana na ushindi wake wa kushangaza dhidi ya Hillary Clinton uchaguzi wa urais nchini Marekani mwezi Novemba.
Bw Trump ameambia kipindi cha Today cha NBC muda mfupi baada yake kutangazwa mshindi kwamba "ni heshima kubwa" na kwamba ina "maana kubwa sana" kwake.
Alichaguliwa kutoka kwa orodha ya watu 11, wakiwemo Bi Clinton na Rais wa Urusi Vladimir Putin.
Kiongozi wa chama kinachopigania uhuru wa Uingereza, Nigel Farage, aliyeongoza kampeni ya Uingereza kujiondoa kwa taifa hilo kutoka Umoja wa Ulaya pia alikuwa kwenye orodha hiyo.
Kwa mujibu wa mhariri mkuu wa jarida la Time Nancy Gibbs, Bi Clinton alimaliza akiwa wa pili.
Anasema ushindi wa Bw Trump ulikuwa jambo rahisi kuamua.
Time wanasema rais huyo mteule ni kama amechora upya sheria na kanuni za siasa Marekani.
Jarida hilo liliwaalika wasomaji kupigia kura mtu waliyeamini alifaa kushinda, lakini uamuzi wa mwisho ulifanywa na wahariri.
Wengine waliokuwa wanashindania tuzo hiyo ni:
  • Mwanasarakasi wa Marekani Simone Biles aliyefana sana michezo ya Olimpiki
  • Wanasayansi wa CRISPR kutoka Urusi, waliovumbua teknolojia ya kuhariri DNA
  • Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan
  • Wakazi wa Flint, Michigan waliofichua kuwepo kwa sumu ya madini ya risasi kwenye maji
  • Waziri Mkuu wa India Narendra Modi
  • Mwansihili wa Facebook Mark Zuckerberg
  • Mwanamuziki Beyonce
Mshindi wa mwaka jana alikuwa Kansela wa Ujerumani Angela Merkel.

No comments:

Post a Comment

Total Pageviews